0
Mahakama moja nchini Kenya imemfunga jela Feisal Mohammed, anayetuhumiwa kwa ulanguzi wa pembe za ndovu, kifungo cha miaka 20 gerezani.

Pia Feisal ametozwa faini ya dola 200,000.

Alipatikana na hatia ya kulangua vipande 413 za pembe za ndovu, vyenye thamani ya dola 400,000.

Hakimu Diana Mochache, wa mahakama ya mji wa Mombasa, alisema kuwa ushahidi uliashiria kuwa Feisal ndiye mmiliki wa vipande vya pembe vya ndovu, vilivyopatikana kwenye bohari moja jijini Mombasa yapata miaka miwili iliyopita.


Hakimu alitaja ulanguzi kama uhalifu mbaya, na kwamba walanguzi wa pembe sharti wafungwe ili kukomesha mauaji ya ndovu.

Ameongeza kuonya kuwa ulanguzi usiposimamishwa, huenda vizazi vivayo vikapewa hadithi tu kuhusu jinsi ndovu walivyokuwa, sawa na jinsi vizazi vya sasa vinapewa hadithi za wanyama waliokuwa wakiitwa dinosaur.

Wanne wengine waliokuwa wameshitakiwa pamoja naye Feisal waliachiliwa.

Pembe hizo zilitolewa wakati wa kutolewa kwa hukumu

Lakini mawakili wake Feisal wamesema amebaguliwa Feisal amefanyiwa ubaguzi na uonevu wa hali ya juu, na kamwe hana hatia na kuwa naamini kuna majaji katika mahakama ya juu ambao hawawezi kudanganyika, na wanaweza kutathmini vyema na ushahidi ili kupata ukweli uko wapi.

Kwa hivyo wao watakata rufaa kwenye mahakama kuu.

Feisal Mohammed amekuwa rumande tangu desemba mwaka 2014.

Wakati pembe za ndovu zilipopatikana, aliondoka Mombasa na kutorokea Tanzania, ndipo polisi wa kimataifa Interpol wakamchapisha kama mhalifu anayetafutwa sana na hivyo kukamatwa.

Post a Comment

 
Top