0
MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imetoa mashine 130 za kielektroniki za kutoa risiti (EFDs) kwa Makatibu Wakuu 25 wa wizara zote nchini kwa ajili ya taasisi na mamlaka zao, zenye wajibu wa kukusanya mapato ya serikali ili kuhakikisha wanaokoa mapato ya serikali yanayopotea.

Akizungumza jana Dar es Salaam wakati wa kukabidhi mashine hizo, Kamishna Mkuu wa TRA, Alphayo Kidata alisema kila wizara itapewa mashine tano ili kuboresha ukusanyaji wa mapato.



"Kila Katibu Mkuu tunamkabidhi mashine tano za EFDs zitakazosaidia kuhakikisha serikali inapata mapato yake na hivyo kuokoa mapato ya serikali ambayo yanapotea," alisema na kuongeza:

"Tunatarajia mashine hizi zitatumika mahususi kutolea risiti, hivyo watumishi wote wa serikali ambao wanafanya marejesho ya matumizi mbalimbali wanatakiwa kuambatanisha risiti za mashine za EFDs".

Aidha alisema TRA inaendelea kudhibiti wafanyabiashara wanaokwepa kutumia mashine za kielektroniki za kodi kwa kuwakamata na kuwatoza faini au kuwafikisha mahakamani kwa hatua zaidi za kisheria.



“Lengo letu ni kuhakikisha tunafikia na kuvuka lengo la kukusanya Sh trilioni 15.5 kwa mwaka wa fedha 2016/2017 ambao tayari tumeuanza,” alisema.

Post a Comment

 
Top