0
WATU katika nchi nyingi wana maoni yanayotofautiana kuhusu ndoa za watu wa jinsia moja. Mwaka wa 2015, Mahakama Kuu nchini Marekani ilitangaza kwamba ndoa za watu wa jinsia moja ni halali kisheria katika nchi hiyo. Baada ya muda, watu wengi walitafuta habari hiyo kwenye intaneti. Mojawapo kati ya maswali yaliyoulizwa mara nyingi lilikuwa ni, “Biblia inasema nini kuhusu ndoa kati ya watu wa jinsia moja?”

Biblia haielezi moja kwa moja kuhusu haki ya kisheria ya ndoa kati ya watu wa jinsia moja. Swali la msingi zaidi ni, Biblia inasema nini kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja?

Watu wengi wanafikiri kwamba wanajua jibu hata bila kuchunguza Biblia kwa makini, lakini majibu yao yanapingana! Baadhi ya watu husema kwamba Biblia inashutumu waziwazi ngono kati ya watu wa jinsia moja. Wengine wanadai kwamba amri ya Biblia inayosema “mpende jirani yako” inaunga mkono uhusiano wowote wa kingono. —Waroma 13:9.



BIBLIA INASEMA NINI?


Ni sentensi ipi kati ya hizi unayofikiri kuwa ni ya kweli?


  • Biblia inashutumu ngono kati ya watu wa jinsia moja.


  • Biblia inaruhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja.


  • Biblia inawachochea watu kuwachukia au kuwabagua watu wanaofanya ngono za jinsia moja.


MAJIBU:


  • KWELI. Biblia inasema: “Wanaume wanaolala na wanaume . . . hawataurithi Ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:9, 10) Andiko hilo pia linawahusu wanawake.—Waroma 1:26.


  • SI KWELI. Biblia inafundisha kwamba mwanamume na mwanamke waliofunga ndoa tu, ndio wanaopaswa kufanya ngono.—Mwanzo 1:27, 28; Methali 5:18, 19.


  • SI KWELI. Ingawa Biblia inashutumu ngono kati ya watu wa jinsia moja, haiwatii moyo watu kuwa na ubaguzi, chuki, au kuwatendea vibaya kwa njia yoyote ile watu hao.—Waroma 12:18.[1]


Mashahidi wa Yehova Wanaamini Nini?
Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba viwango vya Biblia vya maadili ndio viwango bora maishani, na wanaishi kulingana navyo. (Isaya 48:17)[2] Hilo linamaanisha kwamba Mashahidi wa Yehova wanaepuka kila aina ya mwenendo mpotovu kingono, kutia ndani ngono kati ya watu wa jinsia moja. (1 Wakorintho 6:18)[3] Wamechagua kuishi hivyo na wana haki hiyo.

Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kufuata ile Kanuni Bora kwa kuwatendea wengine kwa njia ambayo wao wangependa kutendewa
Licha ya msimamo huo, Mashahidi wa Yehova wanajitahidi ‘kufuatilia amani pamoja na watu wote.’ (Waebrania 12:14) Ingawa Mashahidi wa Yehova wanaepuka ngono kati ya watu wa jinsia moja, hawalazimishi watu wengine wafuate maoni yao, wala hawashiriki katika matendo ya uhalifu yanayosababishwa na chuki na hawafurahii wanaposikia matendo hayo. Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kufuata ile Kanuni Bora kwa kuwatendea wengine kwa njia ambayo wao wangependa kutendewa.—Mathayo 7:12.

Je, Biblia Inaunga Mkono Ubaguzi?
Baadhi ya watu wanasema kwamba Biblia inachochea ubaguzi dhidi ya watu wanaofanya ngono na watu wa jinsia yao na kwamba wale wanaofanya matendo hayo hawapaswi kuvumiliwa. Wanadai kwamba, ‘Biblia iliandikwa wakati ambapo watu walikuwa na ubaguzi. Leo, tunaishi na watu wa kila rangi, taifa na mapendezi tofauti ya kingono.’ Kwa maoni yao, kukataa ngono kati ya watu wa jinsia moja ni kama kumbagua mtu wa jamii tofauti na yetu. Je, ulinganisho huo unafaa? Hapana. Kwa nini?

Kuna tofauti kati ya kukataa matendo ya ngono baina ya watu wa jinsia moja na kuwabagua watu wanaofanya matendo hayo. Biblia inawaambia Wakristo wawaheshimu watu wa namna zote. (1 Petro 2:17)[4] Lakini hilo halimaanishi kwamba Wakristo wanapaswa kukubaliana na kila aina ya mwenendo.

Fikiria ulinganisho huu: Wazia kwamba wewe unachukia kabisa kuvuta sigara na hata unajua kwamba ina madhara. Namna gani ikiwa mfanyakazi mwenzako anavuta sigara? Je, utambagua eti kwa sababu maoni yako kuhusu kuvuta sigara ni tofauti na yake? Kujua tu kwamba yeye anavuta sigara na wewe huvuti sigara kunamaanisha kwamba unamchukia? Ikiwa mfanyakazi mwenzako angekuambia uache kuvuta sigara, je, ungemwona kuwa anakubagua au ameshindwa kukuvumilia?

Mashahidi wa Yehova wanaishi kulingana na viwango vya maadili vilivyo katika Biblia. Hawaungi mkono matendo ambayo Biblia inakataza. Hata hivyo, hawawadhihaki wala kuwatendea vibaya watu wanaojiendesha kinyume na viwango hivyo.

Je, Maoni ya Biblia Yamepita Kiasi?
Namna gani watu ambao wana tamaa ya kufanya ngono na watu wa jinsia yao? Je, walizaliwa wakiwa na tamaa hiyo? Ikiwa ndivyo, je, halingekuwa tendo la ukatili kuwakataza kutimiza tamaa yao?

Ingawa Biblia inakubali kwamba mazoea fulani yamekita mizizi ndani yetu, haielezi sababu ya msingi ya watu kuwa na tamaa ya kufanya ngono na watu wa jinsia yao. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba ikiwa tunataka kumpendeza Mungu ni lazima tuepuke matendo fulani kutia ndani kufanya ngono na mtu wa jinsia moja.—2 Wakorintho 10:4, 5.

Huenda wengine wakasema kwamba maoni ya Biblia kuhusu jambo hilo yamepita kiasi. Lakini madai yao yanategemea msingi wa kwamba ni lazima tutende kulingana na tamaa zetu au tamaa ya ngono ni muhimu zaidi hivi kwamba hatupaswi wala hatuwezi kujizuia. Hata hivyo, Biblia inawaheshimu wanadamu inaposema kwamba wanaweza kushinda tamaa zao. Tofauti na wanyama, wanadamu wanaweza kuamua kutotenda kulingana na tamaa zao.—Wakolosai 3:5.[5]

Fikiria ulinganisho huu: Wataalamu fulani wanasema kwamba tabia fulani kama vile jeuri, zinaweza kusababishwa na chembe za urithi. Biblia haielezi moja kwa moja kuhusu chembe za urithi za jeuri, lakini inasema kwamba watu fulani ‘huwa na hasira’ na “mwelekeo wa ghadhabu.” (Methali 22:24; 29:22) Pia, Biblia inasema hivi: “Acha hasira na uache ghadhabu.”— Zaburi 37:8; Waefeso 4:31.

Huenda wengine wasikubaliane na ushauri huo au kusema kwamba hilo ni tendo la ukatili kwa watu wenye mwelekeo wa jeuri. Kwa kweli, hata wataalamu hao wanaoamini kwamba hasira imetokana na chembe za urithi, wanajitahidi kuwasaidia watu wadhibiti mielekeo hiyo.

Mashahidi wa Yehova wana msimamo huohuo kuhusu mwenendo wowote unaopingana na viwango vya Biblia kutia ndani ngono kati ya watu wa jinsia tofauti ambao hawajafunga ndoa. Katika visa hivyo vyote, shauri hili la Biblia linafaa: “Kila mmoja wenu ajue jinsi ya kukiweza chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima, si katika hamu yenye tamaa ya ngono.”—1 Wathesalonike 4:4, 5.

“Wengine Wenu Mlikuwa Hivyo”
Wakristo katika karne ya kwanza walitoka katika malezi na mitindo tofauti ya maisha, na baadhi yao walikuwa wamefanya mabadiliko makubwa. Kwa mfano, Biblia inaeleza kuhusu wale ambao walikuwa ‘Waasherati, waabudu-sanamu, wazinzi, wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili,’ kisha inaongeza: “Wengine wenu mlikuwa hivyo.”—1 Wakorintho 6:9-11.

Biblia inaposema “Wengine wenu mlikuwa hivyo,” je, inamaanisha kwamba wale walioacha kufanya ngono na watu wa jinsia yao hawakuwahi tena kuwa na tamaa hiyo? Hapana, kwa sababu Biblia inatuhimiza hivi: “Endeleeni kutembea kwa roho nanyi hamtatenda tamaa ya kimwili.”—Wagalatia 5:16.

Ona kwamba Biblia haisemi Mkristo hatakuwa na tamaa isiyofaa. Badala yake, inasema kwamba mtu mwenyewe ndiye anayeamua kutotenda kulingana na tamaa hiyo. Wakristo wanajifunza kuzuia tamaa zisizofaa, yaani hawasitawishi tamaa hizo kwa kuendelea kuzifikiria ili wafanye dhambi.—Yakobo 1:14, 15.[6]

Biblia inaonyesha tofauti kati ya tamaa na matendo. (Waroma 7:16-25) Mtu mwenye tamaa ya kufanya ngono na mtu wa jinsia moja anaweza kujidhibiti asiendelee kukaza akili yake katika jambo hilo, kama ambavyo angeweza kujizuia asitende mambo yasiyofaa, kama vile uasherati, pupa na mwelekeo wa kuwa na hasira.—1  Wakorintho 9:27; 2 Petro 2:14, 15.

Ingawa Mashahidi wa Yehova wanadumisha viwango vya maadili vinavyopatikana katika Biblia, hawalazimishi wengine wafuate maoni yao, wala hawajaribu kubadili viwango vya Mungu ili kutetea haki za watu wengine ambao hawafuati viwango hivyo. Ujumbe ambao Mashahidi wa Yehova wanahubiri una faida, na wana hamu ya kuwaeleza wanaopenda kuusikiliza.—Matendo 20:20.

1. Waroma 12:18:“Iweni wenye kufanya amani na watu wote.”

2. Isaya 48:17: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.”

3. 1 Wakorintho 6:18: “Ukimbieni uasherati”

4. 1 Petro 2:17: “Waheshimuni watu wa namna zote.”

5. Wakolosai 3:5: “Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani.”

6. Yakobo 1:14, 15: “Lakini kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi.”

Post a Comment

 
Top