0
Katika safari ya maisha, wakati mwingine binadamu huwa tuna watu tunaowaita maadui wa mafanikio na maisha kwa ujumla. Na mara nyingi watu hawa huweza kuwa ni marafiki, ndugu au jamaa zetu wa karibu sana.



Na inapotokea ukawatambua maadui hawa wa maisha yako, ambao wanasababisha usifanikiwe kwa kawaida huwa tuna hasira nao sana. Inakuwa iko hivyo kwa sababu hao ndio wanaozuia juhudi zetu za makusudi za kufanikiwa kwetu. 


Hivyo kwa misingi hiyo, binadamu hujikuta yuko makini sana na maadui hawa ili wasije wakasababisha ashindwe kusonga mbele. Hujikuta hata kuweka ulinzi au watu wa kumpa taarifa juu ya adui zake wamafanikio.

Lakini pamoja na tahadhari zote hizo ambazo huchuliwa ili kuwajua maadui wako wa maisha, yupo adui mkubwa sana ambae huwa hachukuliwi umakini wowote na adui huyu ndiye husababisha maisha yako yawe magumu.

Hebu tuchukulie ukagundua kwamba adui mkubwa wa maisha yako ni wewe mwenyewe, hapo utafanyaje? Ni ukweli usiofichika kuna wakati hujikuta ni maadui wakubwa sana wa maisha yetu bila kujijua sisi wenyewe.

Inawezekana unajiuliza kivipi unaweza kuwa adui mkubwa wa maisha yako? 

Yafuatayo Ni Mambo Yanayokufanya Uwe Adui Mkubwa Wa Maisha Yako.

1. Kutokubadilika. 
Ili kufanikiwa, unahitaji mabadiliko endelevu na ya kila siku kwenye maisha yako. Kwa mfano, unatakiwa kubadilika kutoka kwenye hali ya mazoea mabaya uliyonayo na kwenda kwenye hali nyingine bora zaidi ya kimafanikio.

Mabadiliko kwenye maisha yako ni muhimu sana yanakufanya ili usidumae kimafanikio. Kwa msingi huo, kila siku unatakiwa kufanya kitu chanya, ambacho kinaweza kikabadili maisha yako leo na hata kesho.

Ikiwa utakuwa hubadiliki, moja kwa moja utakuwa unajitengezea uadui mkubwa wewe mwenyewe kwenye maisha yako. Kwa kifupi, maisha yako na ya familia yako hayataweza kuwa mazuri kama tu hutaweza kubadilika kwa kiasi kikubwa.

2. Kujishusha sana.
Kama kila wakati unafikiri huwezi kufanya kitu fulani au hata ukifanya kitu hicho kitakuwa chini ya ubora, basi wewe ni moja ya adui mkubwa sana wa mafanikio yako .Kujishusha kwa namna yoyote hakufai.

Kwa kuendelea kujishusha kwenye maisha yako hatafika popote. Hiyo ikiwa na maana kwamba hakuna jambo ambalo utajaribu zaidi ya kujiona huwezi. Kama unajishusha sana kwenye maisha yako elewa wewe ni adui wa maisha yako pia.

3. Kutegemea wengine.
Kuna watu ambao wao kila wakati wanategemea wengine kwa kila kitu. Hawa ni watu ambao hawako tayari kufikiri changamoto zao wakiwa wao kama wao. Ni watu wakuangalia kama wakikwama ni nani atawasaidia?

Inapotokea ukawa kama watu hawa, ambapo hata changamoto ndogo hutaki kutatatua unategemea mtu mwingine awe mzazi au serikali akutatulie chamgamoto hizo, elewa pia unafitini maisha yako na pia ni adui mkubwa wa maendeleo yako mwenyewe.

4. Kuamini wengine sana.
Wapo watu ambao kujiamini wao kama wao ni shida. Ni watu ambao hawaamini uwezo mkubwa walionao ndani mwao zaidi wanaamini wengine ndio wanaoweza kufanya jambo fulani.

Ikiwa kama unajiona unaamini watu wengine sana kuliko unavyoweza kujiamini wewe, elewa kabisa nawe pia unatengeneza uadui na maisha yako. Unatakiwa kujiamini wewe ili usiwe adui mkubwa wa maisha yako.

5. Kuogopa sana.
Kuna masemo ‘usemao woga wako nio umaskini wako’. Hii ni kweli kabiasa, kama wewe ni mwoga karibu kwa kila kitu huwezi kuambuliwa lolote katika haya maisha yenye changamoto nyingi.

Maisha yanakutaka uwe jasiri ili uweze kuyashinda , bila kuwa jasiri na ukamua kuendekeza woga, elewa maisha yatakushinda na wewe ndiye utakuwa adui wa kwanza kwa kuharibu maisha yako.
Soma;Maadui Wakubwa Wa Mafanikio Walio Ndani Yako.

6. Kuwaza sana hasi.
Mtu yeyote ambaye kila wakati anawaza hasi, si rahisi sana kwa mtu huyu kuweza kufanya mambo ya kumsaidia kufanikiwa. Hiyo iko hivyo kwa sababu kila wakati atajiona ni mtu asiyeweza kufanya kitu chochote.

Sasa ili uepuke hali hiyo na usiwe adui mkubwa wa maisha yako ni lazima utambue namna ambayo itakusaidia kuwaza chanya kila wakati. Ukifanya hivyo, itakusaidia sana kuweza kufanikiwa.

7. Kusikiliza sana maoni ya wengine.
Njia ambayo naweza kusema ni mbaya ya kuishi maisha yako, ni kule kuishi kwa kutegemea mawazo ya wengine sana kuliko yako. Ili uweze kufanikiwa ni lazima uamini sana kwanza mawazo yako. Hayo ya wengine ni kama nyongeza.

Kama unaishi maisha ya kusikiliza sana mawazo ya watu wengine ni jambo la hatari sana kwako. Kwa kuishi maisha haya inakufanya moja kwa moja kutokufanikiwa kwenye mambo mengi kwa sababu ya kusikiliza wengine tu hata wale wanao kupoteza.

8 . Kutokutaka kukosea.
Hawa ni watu ambao mara nyingi hawataki kufanya maauzi magumu ya kubadili maisha yao kwa sababu tu ya kuogopa kukosea. Kila siku hujikuta ni watu wa maisha yaleyale kwa sababu hakuna hatua kubwa wanayoweza kuchukua ya kuweza kubadili maisha yao.

Inapofika mahili ukawa ni mtu wa kuogopa kukosea huwezi kufanikiwa. Hakuna kitu ambacho unaweza ukakifanya kwa asilimia mia moja bila kufanya kosa lolote. Makosa ni muhimu katika kukua kimafanikio. Kama utaendelea kushikilia kutokukosea basi pia nawe ni adui mkubwa wa maisha yako.

9. Kusubiri mambo yawe mazuri.
Wapo watu ambao wao kila siku wanajipa moyo kwamba siku moja maisha yatakuwa mazuri. Tatizo la watu hawa sio kujipa moyo hivyo, bali tatizo lipo hufanya hivyo huku wakiwa hawachukui hatua yoyote.

Ikiwa inatokea hivyo kwako na unaendelea kujipa moyo kwamba mambo yangu yatakuwa mazuri na huchukui hatua muhimu, wewe unakuwa ni sawa na adui wa maisha yako. Maisha yako hayataki ahadi, yanahitaji uchukue hatua.

Kwa kawaida yapo mambo mengi ambayo yanaweza kutufanya tuweze kuwa maadui wakubwa wa maisha yetu. Miongoni mwa mambo hayo ndiyo kama hayo tuliyokwisha yaangalia kwenye makala haya.

Nikutakie siku njema na ansante sana kwa kutembelea  DAKIKA ZA MADINI kwa ajili ya kujifunza.

Kwa makala nyingine nzuri za mafanikio soma HAPA kuweza kujifunza na kuboresha maisha yako.

Post a Comment

 
Top