0
Ukichukua barafu ambayo ina nyzi joto labda –10c, ukiweka joto ili barafu hii iyeyuke haitayeyuka hapo hapo. Utaweka joto na barafu itaendelea kuwa barafu, kadiri unavyoweka joto, jotoridi la barafu hiyo linaongezeke, kutoka –10c mpaka –1c baada ya hapo inafika nyuzi joto 0c. Hapa kwenye nyuzi joto 0c ukiongeza joto kidogo tu barafu yote inayeyuka kuwa maji.

Ukitaka kubadili maji hayo uliyoyapata kuwa mvuke haitatokea mara moja, utaendelea kuweka joto na utatoka nyuzijoto 0c utakwenda mpaka 10c, 50c, 90c bado hupati mvuke, kumbuka hapa ni nguvu kubwa ya joto unaweka. Nguvu ikiendelea kuwekwa jotoridi linapanda mpaka 99c, na hatimaye 100c ni katika nyuzi joto 100c ambapo likiongezwa joto kidogo tu, maji yanageuka kuwa mvuke.
Hii ina maana gani kwako?



Unaweza kuweka malengo na mipango yako vizuri na kuanza kuifanyia kazi. Lakini licha ya kufanya kazi kwa juhudi na maarifa bado huoni mabadiliko, unakazana kuongeza juhudi bado mabadiliko hakuna. Elewa kwamba nguvu unayoweka ssa haipotei, bali inajijenga nakuwa kubwa zaidi, siku moja utaweka nguvu kidogo tu na maisha yako yatabadilika moja kwa moja.

Kama kwa kutokuona mabadiliko utakata tamaa na kuamua kuacha hapa ndio unapoteza nguvu yote uliyoweka mwanzoni. Yaani ni sawa na kuweka joto kwenye maji halafu yanafikia nyuzi joto 90c na wewe kwa kuwa hujaona mvuke unasema hamna kitu hapa. Unapoacha tu, joto lote la maji linapungua mpaka 20c na hivyo ukitaka kuyageuza tena kuw amvuke utahitaji kuanza tena mwanzo.

Kama utakata tamaa na kuacha kuweka juhudi sasa, utakapokuja kuanza tena baadae ni kama utaanza upya. Kama utakata tamaa na kuona biashara yako haiwezi kutengeneza faida. Utakaporudi baadae na kuanza upya itakuwa ni kama unaanza upya, utaanza tena kupitia zile hatua za kuweka nguvu bila ya kuona mabadiliko na kama ukiendelea ndio hatimaye unaona mabadiliko.

Watu wengi tumekuwa tukifikiria kwamba unapoamua kufanya mabadiliko basi mabadiliko hayo yanatokea mara moja. Hii sio kweli kabisa, unahitaji muda ili uweze kuyaona mabadiliko haya. Na muda huu sio kwamba unaupoteza bali unauwekeza na unakuwa hazina kubwa sana kwako mbeleni.
Mfano wa Warren Buffet,

Warren Buffet ni mmoja wa watu matajiri sana duniani, alipata utajiri wake kupitia uwekezaji. Sasa hivi utajiri wake unakadiriwa kuwa dola bilioni 63.3. Warren alinunua hisa yake ya kwanza akiwa na miaka 11, sasa hizi ana miaka 84, lakini cha kushangaza ni kwamba asilimia 99 ya utajiri wake aliupata baada ya kufikisha miaka 50. Katika utajiri wa dola bilioni 63.3 alionao, dola 62.7 alizipata baada ya kufikisha miaka zaidi ya 50. Hii ina maana kwamba kwa miaka karibu 30 aliyokuwepo kwenye sekta hii ya uwekezaji hakuona mabadiliko makubwa. Lakini yeye aliendelea kuweka juhudi akijua kwamba siku moja mambo yatakuwa mazuri. Juhudi hizi hazikupotea bure, kwani baada ya kipindi kirefu imekuwa rahisi kwake kuongeza utajiri wake ndani ya muda mfupi. Kwa mfano mwaka 2013 tu wenyewe alitengeneza dola bilioni 12.7. Unaweza kuona hali ilivyo hapa, mtu huyu alifanya kazi kwa juhudi na maarifa kwa miaka 30 akaishia kutengeneza dola chini ya bilioni moja, lakini muda mrefu baadae kwa mwaka mmoja anatengeneza dola bilioni 12.7.

Uvumilivu ni muhimu sana ili kufikia mafanikio

Kitu kikubwa kitakachokufikisha kwenye mafanikio sio muda, juhudi au uwezo. Kitakachokuwezesha kufikia mafanikio makubwa ni msukumo wa ndani ambao unaendeshwa na uvumilivu. Msukumo huu na uvumilivu ndio unaokuwezesha kutumia muda, juhudi na hata uwezo wako mkubwa kufikia mafanikio makubwa. Kuna vikwazo vingi sana kwenye safari ya mafanikio, bila ya uvumilivu, haijalishi una juhudi au uwezo kiasi gani, utashindwa kufikia mafanikio.

Tukiangalia maisha ya watu wengi waliofanikiwa kwenye kada mbalimbali, wote wana kitu kimoja, UVUMILIVU. Watu hawa kuna kipindi walikutana na vikwazo vikubwa ambavyo viliwarudisha wengine nyuma ila wao waliweza kuvumilia na kuendelea.

Hakuna kitu chochote duniani kinachoweza kuchukua nafasi ya uvumilivu, kipaji hakiwezi, dunia imejaa watu wengi wenye vipaji ila hawana mafanikio. Elimu haiwezi, dunia imejaa wasomi wengi ambao hawajafikia mafanikio. Uvumilivu na kujua ni nini unataka ndio nguzo kuu ya kukufikisha wewe kwenye mafanikio.

Wakati unapokutana na changamoto au vikwazo, wakati unapokatishwa tamaa na wakati unapoona mambo hayaendi tena hapa ndio pa kukumbuka kwamba hakuna kitu kiinachoweza kuchukua nafasi ya uvumilivu. Endelea kuvumilia na kung’ang’ania na mwishowe utafikia mafanikio makubwa.
Mwaka huu 2015 amua kung’ang’ania kitu kimoja mpaka uone mabadiliko kwenye maisha yako.


Post a Comment

 
Top